Mapema leo, tarehe 4 Desemba 2025, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Geita, Ndugu Yefred Myenzi, ameongoza kikao maalum kilichofanyika katika Hospitali ya Manispaa ya Geita kwa lengo la kusikiliza na kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili watumishi wa idara ya afya. Kikao hicho ni sehemu ya ziara yake maalum ya kuzunguka katika vituo mbalimbali vya kutolea huduma za afya kusikiliza kero za watumishi.
Akizungumza katika kikao hicho, Mkurugenzi amewapongeza wahudumu wa afya kwa namna wanavyotekeleza majukumu yao kwa weledi na bidii, hali inayochangia kuifanya hospitali hiyo kuendelea kupata sifa chanya kutoka kwa jamii. Amehimiza umuhimu wa kuzingatia sheria, taratibu, kanuni na miongozo ya utumishi wa umma, huku akisisitiza nidhamu binafsi na mahala pa kazi.
Mkurugenzi amekazia zaidi suala la kuwa na kauli njema kwa wagonjwa, akisema huduma bora huanza na lugha nzuri. Amehimiza pia mahusiano mazuri miongoni mwa watumishi, si kazini tu bali pia katika maisha ya kila siku majumbani.
Katika kuhitimisha hotuba yake, Mkurugenzi amewashauri watumishi kujipenda na kutenga siku maalum ya kujipongeza na kuupa mwili pole kama sehemu ya kuongeza morali kazini. Pia amepongeza matumizi ya mfumo wa GoT-HoMIS, na kuwasihi kuendelea kuutumia kwa ufanisi, pamoja na kutunza vifaa tiba na dawa.
Kwa upande wake, Afisa Utumishi wa Manispaa ya Geita, Bi. Ella Makese, aliwapongeza watumishi wa idara hiyo kwa kazi kubwa wanayoifanya, huku akiwataka kutozivumilia changamoto wanazokutana nazo kazini. Alisisitiza kuwa ofisi yake ipo wazi kwa yeyote mwenye changamoto ili kupata suluhisho stahiki kwa wakati.
Naye Mganga Mkuu wa Manispaa ya Geita, Dkt. Sunday Mwakyusa, alimshukuru Mkurugenzi kwa namna ambavyo amekuwa bega kwa bega na idara ya afya, na zaidi kwa namna alivyowasikiliza watumishi moja kwa moja. Alimwomba Mkurugenzi aendelee kufanya ziara kama hizo mara kwa mara katika hospitali hiyo na kwenye vituo vingine vya kutolea huduma za afya.
Geita Tanzania
Sanduku la Posta: P.o Box 384 Geita
Namba ya Simu: 0282520437
Mobile:
Barua pepe: td@geitatc.go.tz
Hatimiliki 2017 Halmashauri ya Mji Geita . Haki zote zimehifadhiwa